Sunday, October 24, 2010

TUNAMTANZANISHAJE MTANZANIA?

“Ili tuendelee tunahitaji vitu vinne: WATU, ARDHI, SIASA SAFI NA UONGOZI BORA”


Maneno haya yaliyoandikwa na waasisi wa Azimio la Arusha. Tuliyaimba na kuyakariri kama kasuku enzi za ujana wetu. Tuliaminishwa na kufahamishwa kwamba hayo manne ndiyo misingi ya maendeleo. Kwamba tuliyakubali na kuyaelewa hayo hilo ni jambo lingine, ila ukweli ni kwamba tulifundishwa na kutakiwa kuamini hayo. Mimi binafsi bado ni muumini wa misingi hiyo ya maendeleo ya taifa ambalo linataka maendeleo ya watu kama alivyotufundisha Baba wa Taifa, na siyo ya vitu.

Mengi yameandikwa na kufanyiwa utafiti juu ya misingi hiyo ya maendeleo. Tunajua mengi kuhusu utajiri tulio nao juu ya ardhi yetu na chini yake; tunajua hata utajiri ulioko majini kama ziwani na baharini. Wasomi wanajua na wanafanya utafiti juu ya siasa na uongozi unaofaa kwa ajili ya nchi yetu kwa kipindi hiki cha soko huria. Tunajua mengi na tunatafiti mengi juu ya misingi hiyo ya maendeleo. Lakini je tumeweza kujiuliza kama kuna watu ambao maendeleo hayo yanawalenga au tunachukulia kivyepesivyepesi kwamba wapo ili mradi tunayo idadi fulani ya wakazi juu ya ardhi hii? Kinachomfanya mtu awe Mtanzania ni nini? Ni kule kuzaliwa na kukulia kwenye ardhi ya nchi inayotambuliwa kwamba ni Tanzania? Je mtu huzaliwa akiwa raia wa nchi fulani au hufundwa kuwa raia wa nchi husika? Hayo ni maswali yanayonitinga ninapotafakari mstakabali wa nchi yetu.


Mimi si shabiki wa siasa za kivyama. Mara ya kwanza na ya mwisho kuhudhuria kampeni za kisiasa kabla ya mwaka huu, ilikuwa ni mwaka 1975 nilipokuwa napiga kura kwa mara ya kwanza. Kulikuwa na wagombea wawili mmoja ana alama ya jembe na mwingine ya nyumba. Sikumbuki nilimpigia kura mgombea yupi kati ya hao wawili. Wakati huo nilikuwa Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Chama kwa tiketi ya Vijana wa TANU, tawi la Kaisho kule Karagwe. Hizo zilikuwa siku za ujana wangu ambapo nilipikika nikaiva kisiasa. NiliTANUishwa, nikaTANZANishwa. Nikapewa mafunzo na maono kuhusu nchi yetu. Watanzania wote, wake kwa waume, vijana kwa wazee, tulioneshwa lengo: Ujamaa na Kujitegemea. Tuliambiwa tusiwe kupe kuwanyonya wengine ili tuishi, bali tujitegemee. Tulipewa matumaini kwamba kwa pamoja tutafika kule tunakotaka kufika kwenye Ujamaa na Kujitegemea. Tulipewa shauku na hamu ya kuishi ili tufike huko. Tulijivuna kuwa Watanzania.

Wakati huo yule aliyetayarishwa kumtanzanisha mtoto wa kitanzania (Mwalimu) hakupelekwa kwenda kusoma kwenye Chuo cha Ualimu kama ilivyokuwa zamani kabla ya kuzaliwa taifa la Tanzania, bali alipelekwa kwenye Chuo cha Elimu ya Taifa. Ajifunze namna ya kumpa fundo mtoto wa kitanzania la kuwa Mtanzania anayeishi na wengine kwa kufanya kazi inayomfanya ajitegemee. Wakati huo tulitambua umuhimu wa elimu inayomkomboa mtu kwa kumfanya ajitambue yeye ni nani na pale pale awatambue wengine ambao si kama yeye bali na wao wapo katika uso wa dunia hii. Je? tumerudi kulekule kwenye chuo cha ualimu ambao hauna utaifa?

Maendeleo ni ya Watu na si ya vitu, anatuasa Mwalimu. Ni mtu wa namna gani ambaye anaweza kuhodhi maendeleo? Kwa maoni yangu, ni yule ambaye amefahamishwa, akapewa uwezo wa kuchanganua, kushakia yaani kutilia shaka kile anachokiona na kuambiwa ili apate kujua kwa kutumia ubongo wake uliochemka na siyo ule ulioganda kwa mapokeo ya kwa kuambiwa tu. Ni yule ambaye anajua anachojua na kujua ujinga wake yaani kile asichokijua. Huko ndiko kuondokana na ujinga ambao enzi za Mwalimu hakukuishia darasani bali ilikuwa ni kazi ya maisha yote. Kisomo chenye manufaa (cha watu wazima) kilitaka kuleta changamoto hiyo!

Kuhesabu vyumba vya madarasa, barabara za lami n.k, ni safi kabisa. Lakini je, wenye hizo barabara na shule wanajua kwamba ni zao au wanaaminishwa kwamba ni kazi ya serikali? Elimu ya kweli inapaswa kumwonesha, kumfahamisha raia, (na siyo mwana wa nchi,) kwamba vile vitu ni vyake: vimetokana na juhudi zake, na utashi wake wa kutaka kutoka pale alipo ili afike pahali pazuri zaidi. Je Mtanzania wa leo anajua na kuamini kwamba hivyo viashirio vya maendeleo ni vyake? Au anaamini na kuaminishwa kwamba vimeletwa? Kama vitu hivyo vinavyoashiria maendeleo vingekuwa vya watu, watu wale wasingekuwa wanaomba serikali iwajengee shule, iwajengee barabara, iwaletee maji nk. Wangepanga wenyewe, wakaamua wenyewe na kuitaka serikali (siyo kuomba) itekeleze hayo. Kwa raia ambao wamefundwa, hiyo ni haki yao ambayo wanatakiwa kuidai, na kwa serikali inayotokana na watu (raia) huo ni wajibu wao ambao wanatakiwa kuutimiza.
Yote haya yanawezekana kama tuna elimu inayomfanya mtu (Mtanzania) ajitambua. Atambue yeye ni nani? Kwamba ni raia wa nchi hii, mwenye wajibu na haki ya kuishi, kufanya kazi na kushirikiana na wenzake kwa manufaa yake binafsi na yale ya taifa lake. Huo ndiyo msingi mama wa elimu, uhuru na maendeleo: KUJITAMBUA (self-consciousness)

Inasikitisha kufuatia kampeni zetu za kisiasa. Kuna vijana wengi ambao wanahudhuria kampeni hizo. Lakini nyingine ni burudani tu. Badala ya kuwaamsha watu ili wajitambue kwamba sasa ni wakati wao kama raia wa kupanga mstakabali wa nchi yao, kwamba nchi inawategemea wao kuijenga, kuchagua nani wa kuwaongoza kuelekea kule ambapo wanaoneshwa; wanaimbiwa ngojera za kuletewa maendeleo. Tangu lini maendeleo ya watu yakaletwa kwa watu?
Najiuliza hivi kweli tunawatendea haki vijana wa nchi hii? Je tunawapa elimu inayowakomboa ili wadadisi mambo, wawe watundu wa fikra kwa kutunduiza fikra? Sina uhakika.

Bila kuwapa hayo: matumaini, maono na taswira; vijana wetu watatupiga mawe kwa haki kabisa. Tunawaboa!

Na Jason Ishengoma,Phd

KWA WALIMU WOTE

Sikilizeni walimu wenzangu mwito kutoka kwa Mwalimu mwenzetu. Mwito wa kututoa katika dimbwi la usingizi. Nadhani ni Mwalimu tu anayeweza kujua na kueleza kilio cha wenzie. Tumsikilize kwa makini Mwl. E. Kezilahabi. Haya siyo maneno wala mawazo yangu. Ni mawazo ya Mkereketwa anayefikiri juu ya hatima ya nchi isiyojali wakunga wake: Walimu.


Sikilizeni wimbo huu:
Nilipokuwa mtoto niliitwa Chacha
Kwa matamshi yangu ya sasa
Nilipokuwa kijana niliitwa Chaupele
Nilipokuwa mtu mzima niliitwa Manywele
Nilipokuwa Mwalimu nikaitwa Bure.

Huu utakuwa wimbo wako
Utakapostaafu urudipo nyumbani
Umelewa kangara na nyayo zako
Zikishindwa kulenga njia nyembamba vijijini.
Utakuwa kichekesho cha watoto
Watakaokuita, Ticha! Popote upitapo.

Kumbuka Mwalimu utakapostaafu.
Mijusi watataga mayai ndani ya viatu
Vyako vilivyokwisha visigino
Na ndani ya sidiria chakavu
Zilizoshikizwa kamba kwa pini.
Mende watazaliana ndani ya chupa tupu
Za marashi na za bia.

Na manyigu yatajenga ndani ya kofia
Zilizosahaulika kutani.
Utakapokufa nge watazaliana
Chini ya jiwe juu ya kaburi lako,
Na mlevi fulani (isome fisadi) akipita atapenga
Na kupangusa vidole kwenye jiwe pweke.
Mwanzo na mwisho wako ndio huo.

Lakini wakati ungali hai
Unaweza kubadilisha mkondo wa maji.
Lakini kwanza tuzungumze. Wewe na mimi.
Acha mioyo yetu izungumze.
Baada ya kunyanyaswa
Na kisha nusu mshahara.

Utafundisha tena nyimbo kuwasifu viongozi?
Utafundisha tena ngonjera?
Utapeleka tena wanafunzi asubuhi
Wakijipanga barabarani kusubiri
Mgeni afikaye saa kumi, na apitapo
Apunga tu mkono kuwatia kichaa cha shangwe
Na huku nyuma mwasambaa na njaa?

Tazama hilo rundo la madaftari mezani
Utamaliza kwa mshahara mkia wa mbuzi?
Tuzumgumze. Ninyi na mimi.
Acha mioyo yetu izungumze.
Mkiwa waoga na kujikunja kama jongoo
Mtawekwa kwenye vijiti na kutupwa
Nje ya ua, na ndani mtawaacha
Wacheza ngoma wakitunga nyimbo mpya.

Sikilizeni walimu.
Anzeni kufundisha hesabu mpya:
Mjinga mmoja kujumlisha na wezi (mafisadi) ishirini
Ni sawa na sifuri.
Fundisheni historia mpya:
Hapo zamani za sasa
Hapakuwa na serikali.

Sikilizeni kwa makini.
Umoja hatuna:
Twasambaratika kama nyumbu.
Tulichonacho ni woga,
Na kinachotuangusha ni unafiki.
Lakini tusikate tamaa kama mbuni.
Tukiupata umoja bado tunayo silaha.
KURA.

(Kezilahabi, Dhifa, Vide-Muwa publishers, Nairobi. 2008)

Walimu wenzangu, tunalipeleka wapi taifa kwa woga wetu? Kweli tunaliunda taifa la kesho la kuigwa? Kwa nini tunafanya mauaji kwa taifa tukijua kweli kwamba tunayofundisha hayawezi kuwapeleka watoto wetu popote na hii inasababishwa na mafao duni yanayotufanya tukimbilie mitaani kutafuta riziki ya kutufikisha mwisho wa mwezi? Tunayo silaha, katuasi Mwalimu mwenzetu. KURA

Jason Ishengoma,Phd

Saturday, October 23, 2010

UHURU WETU NI UTASHI AU NI KUBURUZWA?

. “Uhuru hupatikana kwa kuutoa uhai wako.(kujitoa mhanga) Mtu ambaye hajathubutu kujitoa mhanga, yaani kuutoa uhai wake, anaweza kweli kujidai kwamba anatambuliwa kama mtu, lakini hakufikia ukweli wa utambuzi huo kama nafsi huru inayojifahamu.”
(Phenenomelogy of Spirit. # 187)

Maneno hayo nimeyanukuu kutoka katika kitabu cha mwanafalsafa wa kijerumani, Hegel kutoka katika kitabu cha “Mwonekano wa Roho”. Hegel aliandika kitabu hicho wakati mabomu ya Napoleon Bonapatre yanalindima katika mji wake wa Stuttgart 1807.
Vita vya Napoleon vilikuja baada ya Mapinduzi ya Ufaransa ambayo yaliwatimua watawala wa nchi hiyo iliyoongozwa na mfalme Louis wa 16. Pamoja na kwamba mfalme huyo alikuwa na maaskari na vifaa vya kumlinda, hakuweza kushindana na nguvu za umma uliochoka kwa udhalimu na ukandamizaji pamoja na maisha magumu yaliyotokana na maisha ya anasa ya watawala wa wakati huo.

Tumo katika kipindi cha kuelekea uchaguzi. Ni kipindi ambacho tunaambiwa ni muhimu katika utekelezaji wa kile ambacho wale waliotufinyanga wanakiita Demokrasia. Kwao hao Wafinyanzi wetu demokrasia ina maana ya utawala unaotokana na wengi badala ya wachache wanaojiona kama vile ni wateule wa Mungu. Tunaaminishwa kwamba demokrasia ni ya wote na katika utekelezaji wake baadhi wanaweza kuwakilisha wengi.

Hayo yote sina ugomvi nayo maana tumo katika mkondo wa kileo au kisasa. Tatizo langu ni pale ninapotaka kuswali namna tunavyolielewa wazo zima la demokrasia. Katika nchi yetu kumekuwa na mfumo unaoifanya nchi iwe kama kaya, na yule anayepewa kuongoza nchi, na siyo kutawala, anajiona kama mkuu wa kaya. Kuelewa, kutumia na kuendekeza dhana ya kiongozi wa nchi kama baba mwenye nyumba ni kurudisha nyuma fikra zetu na kutotaka kuelewa nchi au dola ina maana gani katika fikra zetu Waafrika na hata katika fikra za wafinyanzi wetu. Baada ya Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhutubia wazee wa Dar-es-Salaam kwa ukali kuhusu mgomo wa wafanyakazi uliotaka kuitishwa, baadhi ya Watanzania walitafsiri hotuba hiyo kama ya baba mwenye nyumba ambaye amekasirishwa na watoto wake. Kwa fikra zangu, hata raisi mwenyewe alipokuwa akihutubia alifikiri anawahutubia walio chini ya himaya yake. Hakuhutubia kama vile wale ni wabia wenzake waliopewa majukumu tofauti na mwajiri namba moja yaani UMMA.

Fikra hizi za kuona nchi kama mwendelezo wa kaya, na napenda kutumia neno kaya na siyo familia, zimo katika vichwa vya watu kwa muda mrefu sana. Plato katika maandishi yake ya “Republic”, anaiona nchi kama mwendelezo wa kaya. Ndiyo maana anaona mpangilio wa nchi au dola lazima ufuate ule wa kaya. Baba ni kichwa na mfikiriaji; mama ni kifua chenye upendo anayewalea watoto; watumwa, ambao wakati huo walikuwa sehemu muhimu ya kaya, ni miguu na mikono ya kufanya kazi ili kila mmoja apate riziki yake. Kwa mawazo ya Plato nchi inapaswa kuwa hivyo: ni kaya kubwa zaidi. Kila mmoja kwa nafasi yake kadri ya uwezo alio nao. Si Plato tu, Mwalimu Nyerere katika falsafa yake ya Ujamaa hayuko mbali na Plato. Anatumia dhana ya kiafrika ya kaya, ambayo anaisimika katika neno la Kiswahili jamaa linalotoka katika lugha ya kiarabu, na kulitumia kama dhana ya falsafa ya siasa ya kiafrika.
Fikra hizo ziliendelea kutawala kwa muda mrefu hadi yalipojitokeza Mapinduzi ya fikra na siasa ya kileo ambapo dhana ya Kujiendesha (uhuru) inatawala. Katika dunia ya leo ambayo ilijionesha dhahiri katika ulimwengu wa kimagharibi kwa Mapinduzi ya Ufaransa, fikra ya kujiendesha, na siyo kujitawala, ndiyo mhimili na maelezo ya maisha ya watu.
Kwa nini fikra ya kaya haiwezi kuhimili vishindo vya fikra za kileo? Kaya ni mkusanyiko wa watu ambao unatokana na ulazima wa uhalisia au maumbile kinyama. Watu kama watu, [na siyo kwa kuwaita Bin Adam kama vile Binti Adam hawana lao katika kusanyiko hilo], huanza mkusanyiko wa kikaya kwa vile maumbile yanawavuta mwanamume na mwanamuke, wote kama wana au watoto, waunganike. Muungano huo siyo wa hiari. Ni muungano wa kimaumbile, wa lazima. Katika muungano wao huo, huzaa watoto ambao nao aidha ni wake au ni waume. Muungano wa kikaya, ni muungano wa lazima siyo muungano wa kujiendesha (huru). Fikra ya kujiendesha haiwezi kuwemo katika fikra ya kaya. Katika kaya hakuna utashi; kuna ulazima. Hakuna aliyechagua kuzaliwa katika kaya fulani, hakuna anayechagua baba au mama au kaka au dada. Unajikuta katika kaya hiyo na hauna utashi wala uchaguzi.

Katika dunia inayoendeshwa na dhana ya kujiendesha, dhana ya kaya inapotosha ukweli na kufanya fikra zetu zigande. Na katika mgando-fikra huo wa kutotaka kudadisi, kuchambua na kupekuapekua masimulizi (historia), watawala wetu wanapata mwanya wa kujifanya miungu na kututawala. Tunachohitaji katika nchi inayojiendesha, ambayo kwa maneno ya kila siku mmaiita huru, ni viongozi, wanaotuongoza kuelekea kule tunakotaka kuelekea: wanaosimama na sisi wakiwa mbele katika kujiendesha na siyo kuendeshwa. Uongozi huo unawezekana pale ambapo watu wanaojiendesha wanachagua viongozi wao kwa uhuru. Uchaguzi wa namna hiyo unatokana na UTASHI.

Lakini maisha hayaendeshwi kwa utashi tu. Utashi hauwezi kulima “ulime”, utashi hauwezi kujenga nyumba. Tunahitaji akili pia. Akili, hudadisi, hushakia, hugundua, huhesabu. Akili hupanga. Akili haichagui. Taswira ya akili ni kuona jinsi kitu kilivyo. Akili haiwezi kuchagua kati ya hiki au kile itaona kama ni sawa au si sawa na wala si kama ni kibaya au kizuri. Haiwezi kutaka kufanya jinsi inavyotaka. Akili huogozwa na uhalisia wa kitu kwa jinsi inavyokiangalia na kukiona. Akili inatumika katika kupanga, kutenda jambo au kufanya kitu. Wale wanaotumia akili katika kutenda au kufanya jambo tunawaita Wata-alamu, yaani watu wa taaluma. Utaalam unatokana na elimu inayoleta ujuzi au ufundi, yaani namna ya kufunda vitu; yaani, kuvifanya vitu viwe na umbo au fundo. Katika jamii inayojiendesha ni lazima kwanza mtu ajue anaweza kufanya nini ili kuendesha maisha yake. Anaweza kulisha vipi kaya yake kwa kuzalisha chakula cha kutosha kipindi chote cha mwaka. Anahitaji kutumia akili. Kwa kutumia akili hiyo hiyo, mtu anaona mipaka yake. Anaona kwamba hawezi kwenda mbali kwa kukaa na kaya yake peke yake. Anahitaji kaya nyingine, anahitaji ufundi na ujuzi wa mwingine ili aweze kupata kile anachokitamani na kukipenda. Hapo anatumia utashi wake kuchagua kushirikiana na wenzake ambao siyo wa kaya yake bali wenye kaya zao ili wote kwa pamoja wafikie kile ambacho kila mmoja anakitamani lakini hawezi kukipata akiwa peke yake. Akili inamfanya mtu aone uhalisia wa vitu na utashi unamfanya achague njia ya kufuata ili kufikia lengo lake. Lengo ni kile unachokitamani, kile unachotarajia. Hicho ndicho unachokichagua.

Katika utashi ndimo demokrasia imejikita, ni kuchagua. Uchaguzi unahusu kuchangua wale watakaotuongoza na wala siyo wale watakaotutawala. Kuongoza ni kuonesha njia. Huwezi kuonesha njia kama hujui unapokwenda yaani unapoelekea. Kuishi kwa kujiendesha yaani kwa uhuru ni kujua unakotaka kwenda na kutafuta njia ya kukufikisha kule Ili kuwa na viongozi tunahitaji kujua lengo la watu husika. Kujua njia kunahitaji kutumia akili, siyo utashi. Viongozi pamoja na wale wanoongozwa wanahitaji WAONESHAJI, wanaojua njia ilivyo. Hawa ni Watawala (administrators) na wala siyo viongozi (Leaders). Watawala wana uwezo wa kudhibiti, kufanya vitu viende kwa utaratibu fulani. Wanajua njia, ni wataalam. Lakini je, watu kama watu tunaweza kuwaachia wataalam, watu wanaotumia akili yao tu, kutuonesha kule tunakotaka kwenda bila kuwadhibiti?

Katika ushirikiano wa kileo hilo ndilo lililozaa mgawano wa madaraka katika jamii kati ya Uongozi ambao unapewa Serikali na Utawala ambao unafanya kazi chini ya serikali. Serikali ya watu wanaojiendesha wenyewe, ni serikali inayotokana na watu. Inachaguliwa. Inapochaguliwa serikali hiyo inakabidhiwa watawala, yaani wataalam wa nyanja mbalimbali ili wawafanyie kazi WENYEDOLA, yaani wenyenchi, na siyo tu wananchi, kwa malengo waliyokubaliana. Viongozi wanaokabidhiwa serikali wanawakirisha matakwa au utashi wa wenyedola. Serikali haina dola, inakabidhiwa vyombo, ili ivitumie vyombo hivyo kwa niaba ya wenyedola.

Vyombo vya dola ni vyombo katika maana kamili ya vyombo. Havina utashi wala mamlaka ya kufanya vinavyotaka. Vinafuata matakwa ya wenyedola ambao ni raia wa dola hilo. Lakini katika tabia na mazoea tuliyojiumbia, vyombo vya dola vinaanza kujiona kama vile viko juu ya wenyedola. Kuwaonesha wenyedola mbinu za maguvu ya kuwatishia kama watadai haki yao ya kuchagua wale wa kukabidhiwa mikoba ya kuendesha dola, ni kwenda kinyume na uongozi wa kujiendesha. Wataalm wa kutumia dhana za kudhibiti adui wa dola (jeshi) wako chini ya wenyedola. Jeshi halina nguvu juu ya UMMA. Adui wa umma ni adui wa dola. Na jeshi linalotishia umma limeacha kuwa chombo cha dola. Utawaua raia wangapi wanapoanza kupigana wenyewe kwa wenyewe? Jeshi utakuwa wapi? Nje ya umma au sehemu ya umma?
Serikali yoyote ni mali ya umma, ni mali ya wenyedola. Lakini tumekuwa na kasumba ya kuchanganya serikali na umma. Hata vyombo vya umma, kama vile wafanyakazi, badala ya kuitwa watumishi wa umma (civil SERVANT); watu wa kutumwa na umma, tumewaserikalisha na kuwaita wafanyakazi wa serikali. Tukumbuke kwamba serikali inabadilika kila baada ya uchaguzi. Je? Wafanyakazi hao uwa wanabadilisha mwajiri kila baada ya miaka mitano? Je wafanyakazi wa serikali, wanaajiriwa na nani wakati serikali mpya inapoundwa? Serikali huondoka lakini umma hubaki. Watawala wetu, yaani watumishi wa umma, wangejifunza hilo kwamba anayedumu ni umma na wala siyo serikali, tungepiga hatua. Tungeachana na vitisho tunavyopatiwa wenyedola ambao tumenyanganwa dola au nchi yetu na tukabaki ni wana wa nchi tu: WANANCHI. Tumebakiza haki ya kuzaliwa tu ambayo kama nilivyogusia hapo juu haitupi nafasi ya kujiendesha, yaani kuwa huru. Ni ulazima tu kwamba ni wana wa nchi hii.

Tabia yetu tuliyojijengea ya kuangalia mambo bila kuyadadisi na kuyashakia, ndiyo inayotufanya tutawaliwe na watawala wanaotufanya ni watoto na wao ni baba. Hali hiyo hiyo ndiyo inatufanya watumishi wa umma tujione ni sehemu ya uongozi ambao umejifanya utawala. Mtumishi ni mtaalam, amewekwa pale na wenyedola ili atumike kwa sababu ya utaalam wake na siyo urai wake. Serikali inaongoza wenyedola kwa kupitia watawala ili watawale njia. Lakini kule tunakoelekea tunapataka sisi na wala siyo serikali wala watawala.
Serikali yoyote ni wapangaji katika nyumba inayoitwa taifa na siyo wenye nyumba.
Tuifungue akili yetu ione na iwe huru ili tujiendeshe kuelekea kule tunakakotaka.

Swali: je taifa la Tanzania linataka au linaelekea wapi? Labda kwa kuwa hatuna dira, hatuna mwelekeo, hatujui nani mlenga shabaha mzuri anayeweza kutufisha pale.
Kama mwanafikra nabaki nikiranda katika msitu wa kufikiri: je taifa letu lina Watu ambao kwa mtazamo wa Azimio la Arusha ndiyo msingi wa kwanza wa maendeleo? Je hatuna mkusanyiko wa watu ambao hawana muono wa pamoja hivyo kila mmoja anajali kaya yake na tumbo lake? TUTAFAKARI!


By Dr. Jason Ishengoma.

Sunday, October 17, 2010

Philosophy in East Africa Conference 2010.

The Philosophy Association of Tanzania (PHATA) is organizing the second Philosophy Conference in East Africa to be held at Blue Pearl Hotel in Dar es Salaam,from 18th-20th Nov, 2010.This is a continuation of the Philosophy conference in East Africa – towards critical thinking, professionalism and democracy –event held at Regency Park Hotel (Dar es Salaam, 18th-20th Nov. 2009). The main theme is PHILOSOPHY AND DEVELOPMENT.

The topics include, but not restricted to
1 Philosophy in Africa today
2 Philosophy in Civic Ethics
3 Philosophy and the Youth
4 Unity and Religious Diversity
5 Global and International Justice
6 Issues of Transitional Justice
7 Human Rights from a Global Perspective
8 Philosophy and the Law

The Keynote Speaker will be Prof.Wamba Dia Wamba from Democratic Republic of Congo.


The Conference is hosted by the Philosophy Association of Tanzania (PHATA) in collaboration with –The Philosophy Unit, University of Dar es Salaam, Department of Philosophy and Religious Studies-University of Nairobi Kenya, Department of Philosophy-Makerere University Uganda, Mores –research project / Social and Moral Philosophy-University of Helsinki, Finland.